|
MAOMBI YA MIKOPO YA WANAFUNZI WA ELIMU YA JUU KWA MWAKA WA MASOMO 2013/2014
1.0 Utangulizi
Bodi ya Mikopo inawatangazia wanafunzi wote wanaotarajia kujiunga na Vyuo vya Elimu ya Juu kwa mwaka wa masomo 2013/2014, wanafunzi wanaoendelea na masomo na Umma kwa ujumla, kuwa itaanza kupokea rasmi maombi ya mikopo kuanzia tarehe 1 Mei, 2013.
Maombi ya mikopo yatafanyika kwa njia ya mtandao kwa kupitia anuani ifuatayo: http://olas.heslb.go.tz. Vipeperushi maalum vyenye maelezo ya jinsi ya kuomba kwa njia ya mtandao vinapatikana kwenye Vyuo vya Elimu ya Juu, Ofisi za Elimu za Wilaya, kwa Watoa huduma ya Intaneti, Makao Makuu ya Bodi na kwenye Ofisi za Bodi za Kanda. Maelezo hayo pia yanapatikana kwenye tovuti ya Bodi: www.heslb.go.tz.
Waombaji wapya wanatakiwa kulipa ada ya maombi ya mikopo ya shilingi 30,000/=. Wanafunzi wote walio katika mwaka wa tano au sita wa masomo wanatakiwa kuendelea kulipa ada ya maombi ya shillingi 10,000/=. Wanafunzi wanaoendelea na masomo katika mwaka wa pili, tatu na nne ambao walilipa ada ya maombi ya shillingi 30,000 katika miaka ya masomo ya 2009/2010, 2010/2011 na 2011/2012 HAWATAKIWI KULIPA TENA ADA HIYO YA MAOMBI YA MIKOPO.
Sifa za waombaji ni kama zilivyotajwa katika kifungu cha 17 cha Sheria Na. 9 ya mwaka 2004 (CAP 178) ambazo ni:
(i) Kuwa Mtanzania,
(ii) Kudahiliwa katika chuo cha elimu ya juu,
(iii) Kutokuwa na njia nyingine za kugharamia elimu ya juu
(iv) Kufaulu mitihani ya mwaka uliotangulia (kwa waombaji wanaoendelea na masomo)
(v) Kuwa mhitaji
Aidha, mwongozo na masharti ya utoaji mikopo kwa mwaka wa masomo 2013/2014 utapatikana kwenye Vyuo vya Elimu ya Juu na pia kwenye tovuti ya Bodi (www.heslb.go.tz) baada ya kuridhiwa na Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi.
2.0 Hitimisho
Bodi inasisitiza kwamba waombaji wa mikopo wazingatie muda uliopangwa na pia kufuata kwa umakini taratibu zote zilizoanishwa katika uombaji wa mikopo. Kumbuka hakutakuwa na muda wa ziada baada ya muda uliopangwa kupita.
Mwisho wa kupokea maombi ya mikopo ni tarehe 30 Juni, 2013.
Imetolewa na:
Mkurugenzi Mtendaji
Bodi ya Mikopo ya Wanafunzi wa Elimu ya Juu |