Higher Education Students' Loans Board
TZS 3 Bilioni kusomesha wanafunzi 640
Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Profesa Adolf Mkenda leo Jumanne, Septemba 27, 2022 amezindua rasmi maombi ya Samia Scholarship kwa wanafunzi 640 waliofaulu kwa viwango vya juu katika masomo ya sayansi kwenye mitihani ya kidato cha sita ya Baraza la Mitihani Tanzania (NECTA).
Akisoma tangazo la kuhusu Samia Scholarship mbele ya wadau wa elimu nchini katika ukumbi wa Mikutano uliopo katika Jengo la Ofisi ya Tume ya Uchaguzi, Njedengwa, Dodoma, Prof Mkenda amesema lengo la ufadhili huo wenye thamani ya TZS 3 bilioni ni kuhamasisha wanafunzi wenye ufaulu wa juu katika masomo ya sayansi kidato cha sita ambao wamepata udahili katika vyuo vikuu nchini kusoma kozi za Sayansi, Teknolojia, Hisabati na Tiba.
Wanafunzi hao 640, wavulana ni 396 (62%) na wasichana ni 244 (38%) na watafadhiliwa kwa asilimia 100 kwa kipindi chote cha masomo yao katika vipengele vya Ada ya Mafunzo, Posho ya chakula na malazi, Posho ya Vitabu na Viandikwa, Mahitaji Maalum ya Vitivo, Mafunzo kwa Vitendo, Utafiti, Vifaa saidizi kwa wanafunzi wenye mahitaji maalumu na Bima ya Afya.
Majina ya wanafunzi watakaopata Ufadhiili wa Samia Scholarship yanapatikana kwenye tovuti hii au ya Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia www.moe.go.tz na maombi yatapokelewa kwa siku 14 kuanzia Jumatano, Septemba 28, 2022 kupitia https://olas.heslb.go.tz